Vielezi huwakilishwa kwa herufi E.

Ni aina ya maneno ambayo hutoa maelezo zaidi kuhusu jinsi kitendo kilivyotendeka; yaani zinaeleza zaidi kuhusu vitenzi.

Kwa mfano; Alifika (T) mapema (E).

Kuna aina nne za Vielezi vya Kiswahili:

Vielezi vya Mahali

Vielezi hivi huonyesha mahali ambapo kitendo kilitendeka.

Kwa mfano:

  • Wanafunzi walisoma darasani.
  • Wazazi walilima shambani.
  • Mama alienda sokoni.

Vielezi vya Wakati

Huonyesha wakati kitendo kilitendeka.

Kwa mfano:

  • Mama atarudi jioni.
  • Shule zitafunguliwa mwezi ujao.

Vielezi vya Jinsi.

Vinaonyesha namna kitendo kilitendeka.

Kwa mfano:

  • Aliingia polepole
  • Mzee alifua kivivu
  • Wanafunzi walisoma kimoyomoyo.

Vielezi vya Idadi

Vinaonyesha mara ngapi au kiasi kipi kitendo kimetokea.

Kwa mfano:

  • Mama hufua mara nyingi.
  • Wanafunzi husoma siku zote.